NAMNA YA KUSIKIA NA KUIELEWA SAUTI YA MUNGU ILI IKUSAIDE KATIKA KUFANYA MAAMUZI

 

4

Na: Patrick Sanga

Mada – Njia anazotumia Mungu kusema na mwanadamu (Sehemu ya kwanza)

Katika sehemu ya kwanza na ya pili ya ujumbe huu naliandika mambo muhimu ya kujua kwanza kuhusu sauti ya Mungu. Ili kusoma sehemu hiyo bonyeza link hii https://sanga.wordpress.com/2015/04/08/namna-ya-kusikia-na-kuielewa-sauti-ya-mungu-ili-ikusaidie-katika-kufanya-maamuzi-sehemu-ya-2/ Katika sehemu hii ya tatu na ya kwanza kwa mada hii nitaendelea na somo hili kwa kuanza kunagalia njia ambazo Mungu hutumia kusema na wanadamu, naam sasa fuatana nami tuendelee;
Katika Yohana 5:30 imeandikwa Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama NISIKIAVYO ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka’. Andiko hili linatuonyesha utaratibu au nidhamu aliyokuwa nayo Yesu katika kutekeleza kusudi la kuletwa kwake hapa duniani.
Yesu anatueleza wazi kwamba katika utumishi wake, hakutafuta kutekeleza mapenzi yake, bali kadri ALIVYOSIKIA kutoka kwa baba yake ndivyo alivyotenda. Ushuhuda huu wa Yesu unatufanya tujue kwamba, kumbe sauti ya Mungu ina umuhimu wa kipekee katika kutusaidia kufanya maamuzi mbalimbali yanayotukabili kila siku.
Sauti ya Mungu ni nini? – sauti ya Mungu si tu maneno yanayotoka kwenye kinywa chake kama wengi wanavyofahamu bali ni UJUMBE ambao Mungu analeta kwenye maisha yako kwa NJIA mbalimbali ili kukuondoa kwenye matakwa/makusudi yako na hivyo kukusaidia kuyatenda mapenzi yake makamilifu.
Zifuatazo ni baadhi ya njia muhimu ambazo Mungu hutumia katika kusema, kufikisha ujumbe au kufanya mawasiliano na mwanadamu;
  • Kupitia neno lake
Neno la Mungu ndio msingi mkuu wa Mungu kusema na mwanadamu. Hata njia nyingine ambazo Mungu atatumia kusema na wanadamu ni dhahiri kwamba ujumbe wake lazima uendane na neno lake na si vinginevyo.
Katika 2Timotheo 3:16-17 imeandikwa Kila andiko lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema’.
1
Neno la Mungu ndiyo sauti kuu ya Mungu duniani kwa wanadamu na hivyo kuwa na ufahamu wa kutosha wa neno la Mungu ni lazima kwa mwamini anayetaka kuisikia sauti ya Mungu iliyoko ndani ya neno lake. Kadri mwamini anavyokuwa na neno la kutosha ndani yake, ndivyo anavyojiweka kwenye mazingira sahihi ya kusikia na kuelewa sauti ya Mungu kwenye kila eneo la maisha yako na hivyo kuwa kwenye nafasi bora ya kufanya maamuzi.
  • Kupitia ndoto
Katika Hesabu 12:6 imeandikwa ‘Kisha akawaambia, Sikizeni basi maneno yangu; Akiwapo nabii kati yenu, Mimi, BWANA, nitajifunua kwake katika maono, NITASEMA NAYE KATIKA NDOTO’. Ndiyo, Mungu husema kupitia ndoto, kwa kuwa ndoto ni lugha ya picha tena rahisi ya mawasiliano kwa yeye kufikisha ujumbe wake na hivyo kumsaidia mtu aelewe mpango wake (Mungu) kwenye maisha yake na hivyo kufanya maamuzi muafaka.
Pia katika Ayubu 33:14 imeandikwa ‘Kwa kuwa Mungu hunena mara moja, Naam, hata mara ya pili, ajapokuwa mtu hajali. Katika ndoto, katika maono ya usiku, Usingizi mzito uwajiliapo watu, Katika usingizi kitandani’. Hapa Biblia inatueleza kwamba kumbe ndani ya ndoto kuna sauti na hivyo mtu anaweza kuisikia sauti ya Mungu kupitia ndoto, ingawa si ndoto zote huambatana na sauti. Ndoto huja pale mtu anapokuwa amelala usingizi na hili lina maana, mtu anahitaji muda na mazingira bora ya kulala ili Mungu aweze kusema naye kwa njia hii. Ndoto inaweza kuja kwa mfano wa hadithi au tukio lenye kisa au uzoefu fulani ndani yake.
2

Endapo, katika ndoto ambayo ni ya kutoka kwa Mungu, ukiona unaongea, maana yake Mungu anakuonyesha nini cha kusema, kufanya au kuomba punde utakapoamka. Kuomba baada ya kuamka au kushtuka ni LAZIMA ili kuhakikisha zile za kutoka kwa Mungu zinatimia na zile za kutoka kwa Shetani zinazuiliwa.Jambo la msingi ni lazima mtu ajifunze kutafsiri ndoto anayoiota kama sauti ya Mungu kwa kuwa ndani ya ndoto kuna ujumbe. Kuwa na ufahamu wa kutosha wa neno la Mungu ndio msingi muhimu wa kuelewa na kufasiri ndoto unazoota. Rejea mifano ifuatayo ndani ya Biblia ili kuelewa zaidi njia hii.
Mungu anasema na Abramu kuhusu uzao wake (Mwanzo 15:12), Mungu anasema na Sulemani juu ya mambo mbalimbali (1Wafalme 3:5-13), Mungu anamonya Abimeleki kuhusu mke wa Abramu (Mwanzo 20:1-7), Mungu anamuonya Yusufu, asimwache Mariam (Matahyo 1:20), Mungu anasema na Yusufu kuhusu ulinzi wa Yesu dhidi ya hila za Herode (Mathayo 2:13).
  • Kupitia watumishi wa Mungu au viongozi wa kiroho   
Katika kuzungumza na wanadamu, Mungu amejiwekea pia utaratibu wa kutumia watumishi wake mbalimbali ikiwa ni pamoja wachungaji, manabii, walimu, manabii na mitume au kwa lugha ya ujumla viongozi wa kiroho. Mungu anatumia watu hawa kwa sababu (a) utaratibu aliojiwekea kama nilivyosema awali (b) kutokana na nafasi zao katika mwili wa Kristo na (c) watu wengi hawako tayari kulipa gharama ya kutafuta kuisikia na kuelewa sauti ya Mungu.

3

Watumishi wamewekwa maalum na Mungu kwa ajili yetu ili watusaidie kuelewa mapezi yake kwenye maisha yetu na hivyo kufanya maamuzi sahihi kwa kila hatua. Katika Luka 16:29 imeandikwa ‘wanao Musa na manabii wawasikilize wao’. Naam kwa lugha nyingine Musa na manabii (watumishi) ndiyo sauti ya Mungu kwao.
Hata hivyo ni lazima watu wawe na tahadhari kwamba watumishi wanaolengwa hapa ni wale walioitwa na Mungu kweli, yaani watumishi wa kweli (nuru) na si wa uongo (giza). Tafadhali rejea maandiko yafutayo kwa ufahamu zaidi (1Samweli 2:27, 1Samweli 9:9).
Mungu akubariki kwa kufuatilia mfululizo huu. Katika sehemu ya nne, nitaendelea kuandika njia nyingine ambazo Mungu hutumia kusema na wanadamu

Post a Comment

0 Comments