NGUVU ZA KUVUKIA HATUA NYINGINE



NGUVU ZA KUVUKIA HATUA NYINGINE

“Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo” (Danieli 6:10).

Maisha ni safari ambamo kuna mambo mengi. Sio mara zote mambo yatakuwa mazuri na mepesi. Hata kama unampenda Mungu sana na umeamua kuishi maisha ya kumpendeza siku zote, kuna mapito imekupasa kupita. Uwe makini.
BWANA akijua hayo alisema, “ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; Mimi nimeushinda ulimwengu” (Yohana 16:33). Yeye alishinda, ndio maana amekuwa “hakimu wa haki” kwa maana katika mambo YOTE naye alijaribiwa kama sisi, akashinda (Waebrania 2:17,18). Unapopita katika magumu, jua BWANA naye alipita. Unapokutana na Ibilisi ana kwa ana, jua BWANA naye alikutana na Ibilisi ana kwa ana, tena nyikani (Luka 4:1-13). Jipe moyo, utashinda.

Zingatia jambo hili, kama BWANA alimwambia Petro, mwanafunzi wake ampendaye, “nenda nyuma yangu Shetani” (Mathayo 16:23), kwa sababu ya kauli yake; yaani Petro alitumiwa na Ibilisi wakati huo; imekupasa kujua kwamba, watu wengi walio KARIBU nawe ndio WATAKAOTUMIWA na Ibilisi kukujaribu wewe. Kwa kupitia watu wako wa karibu, utakutana na Ibilisi ana kwa ana! Lile NENO walilitamka masikioni mwako litakujaribu. Je! Utasema UMESABABISHIWA na mtu kufanya ufanyayo? Hukujua unajaribiwa?

Angalia jambo hili, Danieli alipoPITA mahali pa kujaribiwa, kwa NENO la wale watu wake wa karibu kazini [alipokuwa mkuu wa maliwali wa Babeli], hakupambana nao, aliomba mara 3 kwa siku, kama ilivyokuwa destuiri yake. Sasa ona hapa, watu wengi wanapenda kuwa WASHINDI kama Danieli, lakini hawapendi au hawafanyi kama Danieli. Je! Nguvu za Danieli za kuvuka VIKWAZO vyake alipata wapi? Jifunze maisha ya MAOMBI ya Danieli.

Jiulize sasa, Je! Kiwango chako cha maombi ulicho nacho sasa kinaweza KUKUVUSHA unakopita? Je! Kiwango “hicho” kinaweza kukuinua hatua zingine za mafanikio? Jipangie kwa KUAMUA na KUDHAMIRIA kuongeza kiwango chako cha maombi; Mwombe Mungu akusaidie katika nia hiyo. Nakuahidi kwamba haitakuwa rahisi, ila kadri unavyoweka nia na kuanza kuchukua hatua, utaweza kuomba zaidi kuliko mwanzo, nawe utaona utakavyovuka hatua zako kwa ushindi.

Huwezi kuona mahali pameandikwa “Ibilisi akaja kumjaribu Danieli”, lakini nakwambia leo, wale watu aliokutana nao ana kwa ana, kwa kupitia hao, Danieli alikutana ana kwa ana na Ibilisi. Kwa bahati mbaya sana, Ibilisi amepita kwa mke/mume wako hukujua; amepita kwa watoto wako hukujua; amepita kwa wafanyakazi wenzako hukujua; nk. Sasa umebaki na LAWAMA na UCHUNGU na watu, hukujua Adui yako ni MWEREVU kuliko wanyama wote wa walioumbwa! Ubebaki kusema, “kama sio mke/mume wangu nisingefanya haya”, “Fulani ndio amesababisha hata nikawa hivi nilivyo”, “kama sio fulani ningekuwa mbali kiroho”, nk.

UJINGA ukutoke kwa jina la Yesu, utamtwika mwanadamu lawama hata lini na kumwacha Adui yako ali akistarehe bila kuguswa? Utamfanyaje mwanadamu kuwajibika kwa makosa na dhambi zako? Je! hukupaswa kusimama kwanza wewe ili kuwasaidia na wengine?

Shughulika na adui; achana na watu. Hii ni sawa na kulaumu BOMBA kwa sababu hakuna maji. Wengi wa hao unaowalaumu ni kama mabomba tu; aliyekugusa na kukujaribu ni Ibilisi. Shughulika na Ibilisi; hiyo ndio siri ya ushindi wako. Na, Nguvu zako utazipata katika maombi.

Frank P. Seth

Post a Comment

0 Comments