MSAADA KUTOKA KWA MUNGU WA FARAJA



MFALME DAUDI alipatwa na maumivu makali ya kihisia na ‘fikira nyingi zinazofadhaisha.’ Hata hivyo, hakuwahi kutilia shaka kwamba Muumba anatuelewa sana. Aliandika hivi: “Ee Yehova, umenichunguza kabisa, nawe unanijua. Wewe mwenyewe umepata kujua kuketi kwangu na kusimama kwangu. Umeichunguza fikira yangu tokea mbali. Kwa maana hamna neno hata moja katika ulimi wangu, lakini, tazama! Ee Yehova, tayari unajua yote.”—Zaburi 139:1, 2, 4, 23.


Sisi pia tunaweza kuwa na hakika kwamba Muumba wetu anatuelewa na anaelewa jinsi kushuka moyo kunavyoathiri akili na mioyo yetu isiyo mikamilifu. Anajua kinachofanya tushuke moyo na jinsi tunavyoweza kukabiliana na hali za sasa. Isitoshe, ametuonyesha jinsi atakavyoondoa kushuka moyo kabisa. Hakuna mtu mwingine yeyote anayeweza kutusaidia hivyo isipokuwa Mungu wetu aliye na huruma “mwenye kufariji wenye huzuni.”—2 Wakorintho 7:6, Zaire Swahili Bible.

Lakini huenda watu walioshuka moyo wakajiuliza Mungu anaweza kuwasaidia jinsi gani wanapokuwa na hisia zenye kufadhaisha.

▪ Je, Mungu anaweza kufikiwa na walioshuka moyo?

Mungu yuko karibu sana na watumishi wake walioshuka moyo ni kana kwamba anakaa pamoja na “mtu aliyepondwa na mwenye roho ya unyenyekevu, ili kuipa uhai roho ya watu wa hali ya chini na kuupa uhai moyo wa wale wanaopondwa.” (Isaya 57:15) Inafariji sana kujua kwamba “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho”!—Zaburi 34:18.

▪ Walioshuka moyo wanaweza kufarijiwa na Mungu jinsi gani?

Wakati wowote ule, waabudu wa Mungu wanaweza kumfikia “msikiaji wa sala,” ambaye anaweza kuwasaidia kukabiliana na hali na hisia zenye kufadhaisha. (Zaburi 65:2) Biblia inatuhimiza tummiminie yaliyo mioyoni mwetu: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

▪ Vipi ikiwa tunafikiri kwamba sala zetu hazisikiwi kwa sababu tunajiona hatufai?
Kushuka moyo kunaweza kufanya tukate kauli kwamba hatujitahidi vya kutosha kumpendeza Mungu. Hata hivyo, Baba yetu wa mbinguni anaelewa hisia zetu dhaifu, “akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Ingawa “huenda mioyo yetu ikatuhukumu kuwa na hatia,” tunaweza ‘kuihakikishia mioyo yetu’ kwamba “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” (1 Yohana 3:19, 20) Kwa hiyo, unaposali unaweza kutumia maneno kutoka katika mistari ya Biblia kama vile Zaburi 9:9, 10; 10:12, 14, 17; na 25:17.

▪ Namna gani ikiwa tumefadhaika sana hata hatuwezi kueleza tunavyohisi?

Unapolemewa na hisia zenye kuumiza hivi kwamba inakuwa vigumu kuzungumza kwa njia inayoeleweka, usikate tamaa! Endelea kusali kwa “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote,” ukijua kwamba anaelewa hisia na mahitaji yako. (2 Wakorintho 1:3) Maria, aliyetajwa awali katika makala hizi, anasema: “Nyakati nyingine ninapochanganyikiwa sana, huwa sijui nisali kuhusu nini. Lakini ninajua kwamba Mungu anaelewa, naye hunisaidia.”

▪ Mungu anajibu sala zetu jinsi gani?

Biblia haisemi kwamba Mungu anaondoa matatizo yetu yote sasa. Hata hivyo, Mungu anatupa nguvu za kukabiliana na “mambo yote” kutia ndani kushuka moyo. (Wafilipi 4:13) “Ilipogunduliwa kwamba nina ugonjwa wa kushuka moyo,” anasema Martina, “nilimwomba Yehova aniponye mara moja kwa sababu sikudhani ningeweza kukabiliana na hali hiyo. Sasa ninaridhika tu kusali anipe nguvu za kila siku.”

Maandiko ni chanzo muhimu cha nguvu kutoka kwa Mungu ambazo zinawasaidia watu wakabiliane na kushuka moyo. Sarah, ambaye ameugua ugonjwa wa kushuka moyo kwa miaka 35, amejionea faida za kusoma Biblia kila siku. Anasema hivi: “Ninathamini sana matibabu ambayo nimepata. Hata hivyo, ninatambua jinsi kusoma Neno la Mungu kumenisaidia kiroho na kimwili. Nina zoea la kulisoma.”

Watu Hawatashuka Moyo Tena!

Yesu Kristo alipokuwa duniani alitumia nguvu alizopewa na Mungu kuponya magonjwa yenye kuumiza. Yesu alitaka sana kuwapa kitulizo watu waliougua magonjwa yenye kuhuzunisha. Isitoshe, yeye mwenyewe anajua maumivu makali ya kuwa na hisia zenye kufadhaisha. Usiku uliotangulia kifo chake chenye maumivu, “Kristo alitoa dua na pia maombi kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa kutoka katika kifo, pamoja na vilio vyenye nguvu na machozi.” (Waebrania 5:7) Ingawa Yesu alifadhaika sana wakati huo, tunafaidika sasa kwa sababu “anaweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa.”—Waebrania 2:18; 1 Yohana 2:1, 2.

Biblia inafunua kwamba Mungu anakusudia kuondoa hali zote zenye kufadhaisha ambazo husababisha kushuka moyo. Anaahidi: “Mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya; na mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, na muwe na shangwe milele katika hivi ninavyoumba.” (Isaya 65:17, 18) “Mbingu mpya,” yaani, Ufalme wa Mungu, utawezesha kuwe na “dunia mpya,” yaani, jamii ya watu waadilifu duniani walio na afya kamilifu kimwili, kihisia, na kiroho. Magonjwa yote yatafutiliwa mbali kabisa.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Nimeita jina lako, Ee Yehova, kutoka katika shimo la chini kabisa. Uisikilize sauti yangu. Usifiche sikio lako kwa ombi langu la kitulizo, kwa kilio changu cha kuomba msaada. Umekaribia katika siku ile ambayo niliendelea kukuita. Ukasema: ‘Usiogope.’”—Maombolezo 3:55-57

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

‘SEMENI KWA KUWAFARIJI WALIOHUZUNIKA’

Barbara anaposhuka moyo sana na kuhisi hafai kabisa, yeye na mume wake humpigia simu Gerard, rafiki yao ambaye ni mwangalizi Mkristo. Kila mara yeye husikiliza kwa subira Barbara anapolia sana na kumweleza mawazo yaleyale yenye kufadhaisha ambayo amemwambia tena na tena.

Gerard amejifunza kusikiliza bila kuhukumu, kubishana, au kushutumu. (Yakobo 1:19) Kama vile Biblia inavyoshauri, amejifunza ‘kusema kwa kuwafariji waliohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:14) Kwa subira, yeye humhakikishia Barbara kwamba Yehova Mungu, familia yake, na rafiki zake, wanamwona kuwa mtu mwenye thamani sana. Kwa kawaida yeye humsomea andiko moja au mawili, hata ingawa amemsomea baadhi ya maandiko hayo wakati uliopita. Kisha, kila mara yeye husali pamoja na Barbara na mume wake kupitia simu, na hilo huwafariji sana.—Yakobo 5:14, 15.

Gerard anatambua kwamba yeye si daktari na hachukui kamwe daraka la madaktari wa Barbara. Hata hivyo, kwa kuongezea matibabu anayopata, yeye humpa maandiko yenye kuliwaza na sala zenye kufariji, jambo ambalo ni madaktari wachache sana wanaweza kufanya.

Ili ‘useme kwa kuwafariji waliohuzunika’

Unaweza kusema: “Nilitaka tu kukuambia kwamba nimekuwa nikikufikiria sana. Ninajua unakuwa mgonjwa mara kwa mara. Unaendeleaje?”

Kumbuka: Zungumza kwa unyoofu na usikilize ukijiweka katika hali yake, hata kama mtu aliyeshuka moyo atasema mambo yaleyale aliyowahi kusema.

Unaweza kusema: “Ninapendezwa sana na mambo ambayo unaweza kufanya (au “ninavutiwa na sifa zako za Kikristo”) licha ya ugonjwa wako. Hata kama huwezi kufanya mambo yote ambayo ungependa, Yehova anakupenda na kukuthamini, na sisi pia.”
Kumbuka: Uwe mwenye huruma na fadhili.

Unaweza kusema: “Nilisoma andiko hili lenye kutia moyo.” Au unaweza kusema, “Nilikukumbuka niliposoma andiko hili ninalopenda sana.” Kisha soma au unukuu andiko hilo.

Kumbuka: Usizungumze kana kwamba unamshauri.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Faraja Kutoka kwa Maandiko

Lorraine anatiwa nguvu na ahadi ya Yehova katika Isaya 41:10: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.”

Álvaro anasema kwamba maneno ya Zaburi 34:4, 6 humfariji mara nyingi: “Nilimuuliza Yehova, naye akanijibu, naye akanikomboa kutoka katika mambo yote yenye kuniogopesha. Huyu mwenye kuteseka aliita, na Yehova mwenyewe akasikia. Na Yeye akamwokoa kutoka katika taabu zake zote.”

Naoya anasema kwamba kusoma Zaburi 40:1, 2 humfariji: “Nilimtumainia Yehova kwa bidii, kwa hiyo akanitegea sikio lake na kusikia kilio changu cha kuomba msaada. . . . Akazifanya imara hatua zangu.”
Zaburi 147:3 inamhakikishia Naoko kwamba Yehova “anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.”

Maneno ya Yesu katika Luka 12:6, 7 humsaidia Eliz ategemee ulinzi wa Yehova: “Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo, sivyo? Na bado hakuna hata mmoja wao husahaulika mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.”

Maandiko Mengine:

Zaburi 39:12: “Uisikie sala yangu, Ee Yehova, na usikilize kilio changu cha kutaka msaada. Usikae kimya machozi yangu yanapotoka.”

2 Wakorintho 7:6: Mungu ‘hufariji wenye huzuni.’“Zaire Swahili Bible.”
1 Petro 5:7: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu ya Mungu, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’

Post a Comment

0 Comments