SIRI YA MAFANIKIO



‘Siri ya Mafanikio’
Maana ya ‘motivational speaker’ ni msemaji ambaye anawatia moyo watu na kuwahamasisha wafikie malengo au makusudi yao kupitia kubadilisha mtazamo wao. Wanawachochea watu watengeneze malengo (goli) kwa ajili ya maisha yao ya baadaye. Wanafundisha sana juu ya ‘mafanikio’ na wanadai kuwasaidia watu kuboresha na kufanikiwa katika maisha yao.
Usemi au fikra ‘motivational speaker’ inatoka wapi? Inatokana na nia na roho ya kizazi hiki ambao hawamjui Mungu. Nyendo au mafundisho haya yalianza miongoni kwa wasioamini hasa kama miaka 60 iliyopita. Msingi wa mafundisho haya ni ifuatayo: huhitaji mtu mwingine; huhitaji Mungu au dini; wewe mwenyewe kama binadamu tayari unao uwezo ndani yako kubadilisha maisha yako na kutimiza ndoto zako zote na kutekeleza malengo yako yote! Wasemaji hao wanaahidi watu watafanikiwa katika kila eneo la maisha yao – INATEGEMEA NA MTAZAMO NA FIKRA ZAO TU! Ni lazima kubadilisha mtazamo wako tu! Kama ukibadilisha mtazamo wako na fikra zako, yote yatawezekana kwako! Kwa maneno hayo wasemaji hao (motivational speakers) wanachochea hisia za watu ili waamini waweze kutekeleza malengo yao! Wanahubiri maisha ya kujitegemea kabisa! Kwa msingi, wanahubiri wewe ni mungu! Mamilioni wa wasioamini wamefuata ‘injili’ hiyo.
Wasemaji hao wanaandika  ‘Self-help’ vitabu, yaani, ‘Jisaidie Mwenyewe’ vitabu, kama ‘The power of Positive Thinking’, ‘10 Steps to Success’, ‘Achieve Your Goals’, ‘Change your Destiny by Changing your Attitude.’ (‘Nguvu ya Mtazamo Bora’, ‘Hatua Kumi Kufanikiwa’, ‘Tekeleza Malengo Yako’, ‘Badilisha Maisha Yako Kupitia Kubadilisha Mtazamo Wako’ nkd.)
Bila aibu yo yote, wahubiri wa kikristo siku hizi wanatumia maneno haya haya na lugha hiyo hiyo! Ndiyo, wanatumia mistari ya Biblia ambayo wanadhani inatetea mafundisho yao, lakini kwa kufanya hivyo wanaharibu maana ya mistari hiyo tu, kwa sababu kimsingi katika mafundisho ya ‘mafanikio’ lengo lako linapewa kipaumbele cha kwanza na siyo neno la Mungu wala mapenzi ya Mungu. HILO NI KOSA LA KIMSINGI YA MAFUNDISHO YAO. Ni wazi ni lazima kupanga mambo kwa ajili ya maisha yetu. Hiyo siyo tatizo. Lakini neno la Mungu na mapenzi Yake yanapasa yapewe kipaumbele cha kwanza katika yote tunayoyapanga. Wahubiri hao wanaigia wasemaji wale wasioamini (motivational speakers) kabisa na kupitia mafundisho hayo wanataka kuwavuta vijana wengi sana, na wanafanya hivyo! Hasa vijana wa kikristo huvutwa na mafundisho hayo na wanategwa na udanganyifu huo kwa sababu yanaahidi mafanikio na matekelezo ya malengo (goli) yao! Tatizo ni lipi basi? Ya kwanza, watu wengi wanaoyafuata mafundisho hayo hawatafanikiwa kwa sababu mafundisho hayo siyo ya kibiblia. Wanadanganywa tu. Ya pili, kwa nini wengi wanadanganywa kwa urahisi? Kwa sababu mafundisho hayo yanachochea mioyoni mwa watu hamu na hata  uchoyo kwa mambo ya nje ambayo yangewapendeza haijalishi kama ni mapenzi ya Mungu au sivyo. Wanasema, zifuate hatua hizi tu, na utafanikiwa.
Kwenye somo hili nataka kuweka wazi kwamba katika Biblia hakuna ‘motivational speakers’ – hata mmoja! Aidha, Biblia haitumii lugha ya motivational speakers, haitumii ‘filosofia’ ya watu hao. Mapenzi ya Mungu huyapewa kipaumbele cha kwanza katika Biblia.
Yesu Kristo hakuwa ‘motivational speaker’!
Tunasoma kwenye Biblia, “…mtu mmoja alimwambia, ‘Nitakufuata ko kote utakakokwenda.’” Lakini  Bwana Yesu hakujibu, ‘Oh! Nafurahi unapenda kunifuata. Hongera! Kumbe, unavyo vipaji vizuri nami nitakutumia na utafanikiwa!’ Bwana Yesu akamjibu kwa namna hiyo, “Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake.” (Luka 9:57,58). Je, unafikiri jibu hili la Yesu lilimpendeza yule aliyejitolea? Je, maneno haya yalimtia moyo? Kwa maneno haya Bwana Yesu alitaka kumuamsha mtu huyo aelewe kwa dhati maana ya ‘kumfuata Yesu’! Mtu anaweza kuwa na hamu kumfuata Yesu bila kuelewa maana yake, bila ‘kuhesabu gharama’! Labda mtu huyo aliamini Injili ni Injili ya ‘baraka’, yaani, labda akasema moyoni kwake, ‘Ahh, Mungu atanisaidia sasa, atanibariki, ataniokoa kutoka katika mazingira yangu mabaya na atayafanya maisha yangu yawe nzuri na atanisaidia kufanikiwa!’ Jibu la Yesu liliuzima moto wa hamu ya namna hiyo; liliizima hamu yenye tabia ya kibinadamu kujifaidia! Hapana! Injili sio jambo la kujiendeleza mimi mwenyewe, kujifurahisha matelekezo ya malengo yangu, kuboresha ‘uwezo’ wangu, kujitajirisha!
Labda yule aliyetaka kujitolea kumfuata Yesu alifikiri, “Kumbe, ninavyo vipaji, ninao uwezo mzuri ambazo Mungu angeweza kuzitumia kujenga mfalme wake duniani!” Au hudhani hivyo? Lakini nilisoma kwenye Facebook mtu fulani (mkristo?) aliyeweka post ifuatayo kwenye group ya kikristo fulani, “Mungu anautumaini uwezo wako, basi wewe pia unaweza kufanya vile vile.” Na watu wengi (wakristo?) waligonga ‘like’! Tunaongea, tunaandika kama Biblia haipo! Watu hawajali neno la Mungu kabisa! Paulo alitanganza, “Sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti katika nafsi zetu ili TUSIJITUMAINIE NAFSI ZETU, bali TUMTUMAINI MUNGU.” (2 Wakor.1:9), na tena, “Maana sisi tu tohara, tumwabuduo Mungu kwa Roho, na kuona fahari juu ya Kristo Yesu, wala hatuutumainii mwili (yaani, uwezo wangu mwenyewe).” (Wafil. 3:3).
Wengi wanatangaza, ‘Usikate tamaa! Usikate tamaa! Utafanikiwa. Ujitumainie nafsi yako! (have confidence in yourself!). Amini katika uwezo wako na vipawa vyako (believe in your capabilities and gifts!). Songa mbele tu! Mungu atakusaida kufanikiwa!’ Hayo siyo lugha ya neno la Mungu; hayo siyo mafundisho ya maandiko. Na kwa nini wanasema mara nyingi ‘kufanikiwa’? Ina maana ya namna gani? Kufanikiwa katika biashara au kazi yangu? Kwa nini hawatumii lugha ya Biblia? Kwa nini watu hawa hawaandiki ‘Amini Yesu naye atakusaidia kushinda dhambi’ au ‘Usikate tamaa! Songa mbele na utaona Mungu ni Mwaminifu!’ Kwa nini wengi wanapenda na wanapendelea kutumia lugha ya ‘mafanikio’? Kwa nini wanasistiza mambo ya nje tu na siyo mambo ya kiroho? Katika muktadha huo, Bwana Yesu hakutumia lugha hiyo wala mitume Wake.
Bwana Yesu hatafuti watu ‘wajitoleao’ (volunteers). Anatafuta watu ambao watatubu kwa ndani sana, kujikana wenyewe na kuchukua msalaba wao na kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na haki Yake. Mungu anatazamia sisi tuyatafute mapenzi Yake tu, na siyo kuyajenga mapenzi yetu mweyewe kadiri tunavyopenda, kadiri ya ‘uwezo’ wetu.
“Mtu mwingine pia akamwambia, Bwana, ‘Nitakufuata; lakini, nipe ruhusa kwanza nikawaage watu wa nyumbani mwangu.’ (Luka 9:61). ‘Nitakufuata …lakini kwanza…’. Hamna ‘lakini kwanza’, hamna ‘lakini’. Yesu ni Mwana wa Mungu! Huwezi kubadili na Mungu. Yesu hakufa kustarehesha maisha yetu! “Yesu akamwambia, ‘Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu.’” (Luka 9:62).
Unatafuta nini?
Yesu “Akamwambia mwingine, ‘Nifuate’.” Haijalishi unalotaka kufanya au unalopanga. Yesu hakufa kustarehesha maisha yetu au kutimiza mitazamo yetu, alikufa ili tutimize mapenzi Yake ndani yetu kupitia yetu. “Akasema, Bwana, nipe ruhusa kwanza niende nikamzike baba yangu.” Lakini Bwana Yesu hajali mipango yetu, “Akamwambia Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu.” (Luka 9:59,60). Neno la Mungu linakuja kwetu kama neno lenye “nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi KUYATAMBUA MAWAZO NA MAKUSUDI YA MOYO” (Waebr.4:12). Unaona? Watu wengi wanaweza kuwa watu wajitoleao (volunteers) ambao wanafikiri uwezo wao, au vipaji vyao, au ‘maono’ yao, au hata hamu yao kumfuata Yesu zinafaa kwa ajili ya kujenga Mfalme wa Mungu duniani, lakini Bwana Yesu anachunguza na kugundua makasudi ya kiini ya mioyo yetu! Kama ilivyoandikwa, “Kalibu ni kwa fedha na tanuru kwa dhahabu, bali BWANA huujaribu moyo.” (Mithali 17:3). Neno la Bwana linafanya kazi ndani ya mioyo na maisha yetu kama kalibu na tanuru kutofautishiana kati ya maneno na hamu yetu (na yale tunayoyadai), na makusudi yetu kweli kweli!
Unaona? Mtu mmoja anasema, ‘Nitakufuata ko kote utakakokwenda.’ Lakini Yesu alimlazimisha atafakari juu ya gharama ya kumfuata Yeye! Hamu ya kufanya kitu haitoshi! “Kutii ni bora zaidi kuliko dhabihu.” (1 Sam.15:22). Mtu mwingine alikuwa anajishughulisha na jambo fulani lakini neno la Mungu lilikuja kwake kukatiza mawazo na maisha yake! Tunapokuja kwake Bwana Yesu, Yeye hajali mtazamo wangu, au makasudi yangu kwa maisha yangu, au malengo yangu – mambo hayo yote ya kwangu binafsi siyo muhimu kwa ufalme Wake. Msalaba wa Kristo uliyasulibisha mambo haya yote ya binafsi. Sina haki kuwa na makasudi yangu mwenyewe, ndoto zangu za binafsi, kutaka kutekeleza matakwa yangu! Jukumu langu ni “kutoa mwili wangu uwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu.” (Warumi 12:1). Kutoka katika dhabihu hiyo (mahali ambapo sitafuti mapenzi yangu) Mungu ataifufua mapenzi Yake kwa maisha yangu. Ni hatari kwa maisha ya kiroho ukitegemea hamu au uwezo wako kufanya kitu! Bwana anatazamia utii wetu na imani yetu na Yeye atatutia nguvu tufanye mapenzi yake.
NAOMBA UNIELEWE VIZURI. Hapo naongea juu ya wahubiri watumiao mafundisho ya wasioamini (wakati wanadai ni ya kikristo) kuwachochea waumini watufute ‘mafanikio’ badala ya kufundisha neno la Mungu ili kuwapa waumini ufahamu juu ya mapenzi ya Mungu kwa maisha yao. SISEMI huwezi kuchagua upendalo kujifunza juu ya elimu yako. Sisemi ni kosa kuchagua kazi upendayo kufanya! Mambo haya yote ni maisha tu, ni mambo ya kawaida tu – ila kwa wakristo ni jambo la kawaida pia kutafuta mapenzi ya Mungu katika mambo hayo yote kwa sababu ni LENGO letu kumpendeza YEYE katika mambo yote, liwe kubwa, liwe ndogo.
Watu wengi walimfuata Yesu. Je, unafikiri Yeye alikuwa ‘motivational speaker’? Imeandikwa, “Makutano mengi walipokuwa wakifuatana naye.” Na Yesu alifanyaje? Neno la Mungu linatuambia, “aligeuka, akawaambia, ‘Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.” (Luka 14:25,26).
Je, unataka kumfuata?
Je, maneno haya ya Mwana wa Mungu yanakuvuta, yanakuhamasisha (motivate you) umfuate? Au maneno ya Yesu ni changamoto kwako ambayo yanakusababisha utafakari na kuchunguza makusudi yako kweli kweli na kuitafakari  gharama ya kumfuata Yesu? Wapi Bwana Yesu anatumia maneno yafuatayo, “Njoo! Nifuate mimi na utafanikiwa!”, au, “Usikate tamaa. Tengeneza mtazamo wako tu na utafanikiwa”? Hayatumii maneno haya. Badala yake anaendelea kuwaambia watu, “Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.” (Luka 14:27). Inawezekana kabisa watu wengi walimfuata Yesu kwa ajili ya ‘baraka’ na kwa ajili ya miujiza aliyoifanya – na kama wewe ukifanya hivyo, unakosa sana! Kama ukifanya hivyo, mwishoni utakata tamaa, au utachukizwa au hata malengo yako ya binafsi yatakukwaza! Kwa maneno hayo hapo juu, Bwana Yesu alitaka kuweka wazi kabisa ili watu waelewe haitoshi kabisa kumfuata kwa sababu ya ‘baraka’ au ya miujiza au ya ‘mafanikio.’ Ni jambo la kuhuzunisha sana wahubiri wengi siku hizi wanatumia – kwa kusudi – ahadi ya ‘mafanikio’ kuwavuta watu kwa huduma zao na makanisa yao. Wanafundisha kana kwamba ipo ‘siri’ ya mafanikio, na sasa, eti, ili ufanikiwe katika maisha yako lazima ufuate mafundisho yao – badala ya kusoma neno la Mungu tu, badala kuamini neno la Mungu tu, badala ya kulitii neno la Mungu ambalo limeandikwa kwa wazi katika maandiko. Je, neno la Mungu halitoshi kwao?
Changamoto ya mistari hiyo ya hapo juu ni wazi. Lakini kama ukimfuata Yesu, aliahidi ‘tutakuwa na uzima, kisha tuwe nao tele’ (Yoh.10:10), na mambo mengi zaidi. Lakini lengo langu lilikuwa kuonyesha kupitia mistari hapo juu kuwa Yesu hakuwa motivational speaker.
Tafadhali unielewe vizuri. Udanganyifu wa ‘motivational speakers’ ni kama ifuatayo: wanaichochea kwa maneno yao hamu ya ‘nafsi yako mwenyewe’ upate unalotaka, au ufanikiwe au uwe kitu – na wanaahidi mambo haya yote wakati wakidai ni ‘mapenzi ya Mungu’ kwa ya maisha yako! ‘Utafanikiwa! Songa mbele tu! Usikate tamaa! Badilisha fikra zako tu! Utafanikiwa!’ Motivational speakers wanahubiri mambo yale ambayo watu na hata wakristo wengi wanapenda kuyasikia kwa sababu hawahubiri msalaba wa Kristo na kujikana, bali wanahubiri njia kutekeleza makusudi yako mwenyewe ya binafsi, na namna ya kufanikiwa au kutajirika. Kwa hiyo msingi wa mafundisho haya siyo kuyafuata mapenzi ya Mungu bali ‘tekeleze malengo yako mwenyewe, ujipendeze nafsi yako mwenyewe.’
Nijalie nijikatize kutoa maelezo zaidi kidogo juu ya lengo la somo hili:  Ni WAZI katika maisha yetu ni lazima tutafakari na kupanga mambo juu ya mahitaji yetu, juu ya elimu, kazi au biashara zetu. Ni wazi tunapaswa tusiwe wavivu bali  “kwa bidii, si walegevu; mkiwa na juhudi katika roho zenu; mkimtumikia Bwana” (Warumi 12:11). Hiyo ni jambo la kawaida ya maisha! Siyo kosa! Msingi na mzigo wa ujumbe huo ni tuyatafute na kuyafuata mapenzi ya Mungu KATIKA YOTE TUNAYOYAFANYA, na siyo kuyafuata mafundisho (ya wasioamini) juu ya ‘mafanikio’ ambayo yanatupelekea mahali pa kuacha neno la Mungu na badala yake kujenga maisha yetu juu ya mawazo ya wasioamini ambao wanatuchochea tuifuate ‘ndoto’ yetu bila kujali neno wala mapenzi ya Mungu.
Tunapaswa kumfuata na kumwamini Yule aliyesema, “utafuteni ufalme wa Mungu, na hayo mtaongezewa….Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi… Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu…  Umtumaini Bwana ukatende mema, ….nawe utajifurahisha kwa Bwana, naye atakupa haja za moyo wako…. Umkabidhi Bwana njia yako, pia umtumaini, naye atafanya….Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako… Shikeni basi maneno ya Agano hili myafanye, ili mfanikiwe katika yote mfanyayo.” (Matt.12:7,31,31; Wafilipi 4:19; Zaburi 37:3-5; Mithali 3:5-7; Kumbuk. 29:9).
Zaidi ya hayo, neno la Mungu linalsema, “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu IWE DHABIHU ILIYO HAI, takatifu, ya kumpendeza MUNGU, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msiifuatishe NAMNA YA DUNIA HII; bali mgeuzwe kwa KUFANYWA UPYA NIA ZENU, mpate kujua HAKIKA mapenzi ya MUNGU yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.” (Warumi 12:1,2).
Sasa, yeye (mtume Paulo) aliyesema, “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu,” alisema PIA, “Walakini utauwa pamoja na kuridhika ni FAIDA KUBWA. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. Lakini hao watakao kuwa na mali HUANGUKA KATIKA MAJARIBU na TANZI, na TAMAA NYINGI ZISIZO NA MAANA, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi. Bali wewe, mtu wa Mungu, UYAKIMBIE MAMBO HAYO; UKAFUATE haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole.” (1 Tim.6:6-11). Sasa je, unadhani mtume Paulo alikosa aliposema maneno hayo kwake Timotheo? Jibu, moyoni mwako tu. Je, unadhani mtume Paulo kwa maneno yake anawazuia waumini wasiboreshe maisha yao? Jibu moyoni mwako. Je, unadhani, mtume Paulo anataka waumini wabaki hali ya unyonge? Je, Paulo alikosa au hakukosa kwa maneno yake kwake Timotheo? Jibu moyoni mwako – na kama unajibu ‘hakukosa’, unapaswa kutengeneza mtazamo wako, fikra zako na moyo wako uzifanye sawa na Paulo.
Kama tukiongea juu ya maisha yetu, na maisha yetu ya baadaye, kwa nini kwa kiwango kikubwa sana walimu wa ‘mafanikio’ hawanukulu mistari hiyo ya hapo juu katika mafundisho yao?
Wao wanaofundisha ‘mafanikio’ KWA UJUMLA ni nani? Kwa uzoefu wangu wanaishi mjini, siyo kikijini. Kwa ujumla (siyo wote) ni watu wenye elimu, hata elimu ya juu. Kwa ujumla ni watu wanaoishi katika mazingira ambapo FURSA ya kuboresha maisha yao ni zaidi sana kuliko vijijini! Kwa ujumla, sio ‘siri ya mafanikio’ ambayo inawasaidia kuboresha maisha yao, ni fursa ambayo mazingira na familia yao inawatoa! Naongea kwa ujumla. Sisemi kuwa mvivu ni sawa. Hapana, hata kidogo! Lakini wapo wengi vijijini ambao wanayo bidii, na hamu na akili kuboresha maisha yao kadiri wewe unavyokuwa nayo! Nilikutana nao. Lakini fursa ya kuborehsa maisha yao inakosa kwa kiwango kubwa kuliko mjini. Nashangaa sana wao wenye elimu (hata ya chuo kikuu) mjini HAWAELEWI JAMBO HILI LA MSINGI la maisha. Ningeweza kuthibisha ninayoyasema. Wewe unayefuata mafundisho ya ‘siri ya mafanikio’, njoo pamoja nami. Nitakupelekea kijiji mmoja. Kaa pale kwa mwezi moja, au mwezi sita, au miaka sita. Utachoshwa. Hutafanikiwa. Mafundisho yako hayatabadilsha wala kuyagusa maisha ya waumini kwa sababu tayari wengi – hasa vijana – wanayo hamu na bidii na akili kuboresha maisha yao lakini wanakosa fursa kutokana na mazingira yao. SIYO jambo la kutokuchukua fursa waliyo nayo. Hapana. Inatokana na upungufu wa fursa. USIWALAUMU ndugu zako (kupitia ujinga wako) kwa kusema wao ni wavivu, au hawana hamu wala bidii kuboresha maisha yao, au lazima wabadili mtazamo wao. Ni wazi huwajui. SISEMI maisha ya mtu fulani hayawezi kubadilika au lazima abaki yale yale. Hapana. Sisemi hakuna awezaye kuboresha maisha yake, ila mafundisho yako ya ‘mafanikio’ na ‘kubadili mtazamo wako tu’ kwao, hayatawasaidia – unadhihirisha ujinga wako tu juu ya maisha yao na juu ya Biblia!
Ni rahisi. Tunalo neno la Mungu. Wapi katika Agano Jipya mitume waliandika juu ya maskini, ‘badili mtazamo wako tu na utafanikiwa’. (Wanafundisha dhidi ya uvivu na sisi sote tunakubaliana na hiyo). Wapi? SISEMI hali ya mtu fulani haiwezi kubadilika (naomba usinisingize), lakini toa mstari mmoja kwenye Agano Jipya ambao unasema yale yale unavyosema, yaani, ‘badili mtazamo wako tu na utafanikiwa, utajitoa kutoka katika umaskini.’ Toe tu. Jibu ni rahisi – hamna hata mstari mmoja wala mafundisho ya namna hiyo katika Agano Jipya na kimsingi katika Biblia nzima.
Kwa nini nimeandika somo hili? Kwa sababu kimsingi mafundisho ya ‘mafanikio’ yanawaongoza watu ‘kuanguka katika majaribu na tanzi na tamaa nyingi zisizo na maana ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu.’ Basi, mambo hayo ni muhumu sana kwa ajili yetu! Najua watu wale wanadai wanataka kuwasaidia waumini kuboresha maisha yao – lakini huwezi kuwasaidia kwa kutokujali neno la Mungu. Katika mafundisho yote ni afadhali kulitumia neno la Mungu kwa ajili ya maisha ya waumini.
Tuendeleeni sasa na mafundisho. Wengine wanafundisha ni lazima kujipenda mwenyewe kabla ya hujafanikiwa! Hayo ni mafundisho na saikoloji ya wasioamini. Na wahubiri wanapotosha neno la Mungu kwa kunukulu mistari kama Mtt.22:39, “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” Sasa, maneno hayo yanamaanisha? Ina maana ninajipenda mimi mwenyewe, ninajibusu, ninajitazama mwenyewe katika kioo nikisema, “Mimi ni bora, mimi ni mtu wa ajabu! Jinsi ninavyonipenda!” Hasha! Biblia inafafanua Biblia. Mungu apewe sifa! Kama tunasoma Warumi 13:9 na Wagalatia 5:14, tunaona “Mpende jirani yako kama nafsi yako” ina maana USIWATENDEE WATU VIBAYA kwa sababu siyo tabia ya mtu kujitendea vibaya! Hiyo ni maana ya ‘kupenda nafsi yako.’ Kwa mfano, ukijisikia kiuu, utakunywa maji, chai au soda! Ni tabia ya mtu kujitunza na kujilinda mwenyewe. Kwa hiyo katika Warumi 12:20 imeandikwa, “Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake.” Mstari ule hapo juu unahusu MATENDO YETU kwao wengine!
Sasa, kwa nini wanafundisha ni lazima ‘kujipenda mwenyewe’? Kwa sababu wanajua watu na hata waumini wanaweza kujisikia hawafai, na kujichukia mwenyewe. Lakini njia ya kutoka katika hali ya hiyo siyo ‘kujipenda mwenyewe’! Kujisikia wewe hufai ni kazi ya shetani moyoni mwako – njia ya kutoka katika hali hiyo ni kuacha kutokuamini; usipokee uongo wa shetiani; ‘kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Kuvaa silaha zote za Mungu, mpate kuweza KUZIPINGA HILA ZA SHETANI; kuitwaa NGAO YA IMANI, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima MISHALE YOTE yenye moto ya yule mwovu; KULIAMINI pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi. Mwamini Mungu aliyesema, ‘Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa…naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Kwa maneno hayo na mengi mengi zaidi ya maandiko tunaweza kuwatia moyo waumini! Sasa je, kwa nini wale wanaofundisha ‘mafanikio’ hawajali neno la Mungu na badala yake hufundisha mambo matupu na ya udanganyifu kama ‘kujipenda mwenyewe’?
Ninayo raha moyoni mwangu siyo kwa sababu ‘ninajipenda mimi mwenyewe’ (Hasha!), bali kwa sababu Mwokozi wangu alinipenda na alikufa kwa ajili yangu; alinisamehe dhambi zangu zote; alinisafisha kwa ndani na aliweka Roho yake ndani yangu kunifanya niwe mtoto Wake, ‘alinibariki kwa baraka zote za rohoni, katika ulimwengu wa roho, ndani yake Kristo’; na mambo mengi zaidi! Na Yeye ni Yule anayenitia moyo wangu! Sitafuti ‘mafanikio’. Sitafuti kujipenda mwenyewe (Hasha!). Siamini katika mimi mwenyewe (Hasha!). Siweki tumaini langu kwa mimi mwenyewe (Hasha!). I don’t believe in myself – this is idolatry. I don’t trust in myself – this is rebellion against God. Namwamini Mungu. Bwana ndiye tumaini langu! Bwana asifiwe! Namtafuta Yeye ili nimjue Yeye!
Mpendwa msomaji, labda unafikiri ninakwenda kupita kiasi katika ninalosema! Hapana. Mhubiri maarufu mmoja wa Tanzania aliwasisitiza waumini waamue kubadilisha mtazamo wao kwa kusikia yale TU ambayo yatajenga ubora wa maisha yao ya baadaye; akawasisitiza watamani kusikiliza wale watu ambao wamefanikiwa, akidai ‘Imani chanzo chake ni kusikia’. Aliwachochea waumini watengenze goli yao, goli ya achievement akiwauliza wanataka kuwa nani, kufika wapi. Aidha, aliwaambia wachukue kalamu na daftari, kuchora kila saa, mwundo wa serikali yao ya kampuni, namna ya wanataka kuendesha biashara zao, na kuweka pembeni na kurudia tena na tena mpaka wametekeleza lengo lao!
Huo ni mfano wa ‘motivational speaker’. Unapata mafundisho hayo wapi kwenye Biblia? Hayapo. Ni injili ya kujipendeza, ya kujitegemea, kuboresha maisha yako ya nje. Haya ni mafundisho ya saikolojia ya wasioamini wapendao kuboresha maisha yao (bila Mungu) kwa kubadilisha mtazamo wao. Wamefundisha vivyo hivyo (kwa miaka mingi) na wametumia maneno yale yale. Na mhubiri huyo anatumia lugha yao asilimia 100 bila kujisikia aibu!
Inawezekana mhubiri huyo anafundisha neno la Mungu wakati mwingine, lakini hapo anakosea sana. Kwa maneno yake hapo juu anawapeleka watu mbali na neno la Mungu na anawasababisha kuacha njia na nia ya Yesu Kristo. Alisema kwamba ‘Imani chanzo chake ni kusikia.’ Wazo hili peke lake siyo kweli! Analighoshi neno la Mungu. Kujenga imani unahitaji ‘neno la Mungu’. Biblia ianasema yafuatayo, “Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na KUSIKIA HUJA KWA NENO LA MUNGU.” (Warumi 10:17). Unaona? Aliondoa maneno ‘na kusikia huja kwa neno la Mungu’. Na ndiyo kweli, yeye hahubiri neno la Mungu hapo, badala yake anawalisha waumini na mawazo ya wasioamini na saikilogia ya ulimwengu huo. Anachochea wakristo watengenze wenyewe goli yao. Wapi anataja mapenzi ya Mungu? Wapi anasema ‘tujitoe miili yetu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu.’ Wapi anasema, ‘tamani kusikiliza maneno ya Mungu’ au ‘Ishi kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.’ Hamna! Badala yake anachochea mioyo ya waumini wawe na nia ya kujipendeza wenyewe, kuweka malengo ambayo yataboresha maisha, yaani, biashara zao. Kwa kufanya hivyo, anapotosha neno la Mungu na anapotosha watu. “Unataka kuwa nani wewe?” Swali hilo livutalo kiburi na kujitegemea tu! ‘Injili hiyo nyingine’ inataka kunichochea kutengeneze goli yangu kwa kubuni namna gani mimi nataka nifike mahali. Kumbe, sasa wewe ni bwana wa maisha yako!
Kama ukipenda kufanya semina ya uchumi na biashara, fanya semina hiyo kwa kuitumia lugha inayohusu masomo hayo; usipelekee neno la Mungu katika mafundisho yako ya ‘mafanikio’ kana kwamba yanakubaliana.
Najua, ni kweli, kila kazi au biashara inahitaji utaratibu wake na mpango wake, lakini hilo ni jambo la kawaida tu! Na Mungu anaweza kuibariki kazi yako na hata biashara yako – lakini siyo kwa njia ya kupotosha neno la Mungu na kuchanganya neno la Mungu na mafundisho ya wale wapingao Mungu, siyo kwa njia ya kuchochea kujipendeza, uchoyo na hata majivuno. Mafundisho ya neno la Mungu ni tofauti kabisa,
“Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida; WALAKINI HAMJUI YATAKAYOKUWAKO KESHO. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya kusema, BWANA AKIPENDA, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.” (Yakobo 4:13-15).
Hamna ‘Bwana akipenda’ katika mafundisho ya mhubiri yule hapo juu, hamna wazo la ‘mapenzi ya Mungu’. Badala yake waumini wanachochewa kutengeneza malengo ya kuboresha maisha yao kana kwamba ni ‘mapenzi ya Mungu’, au hata kutokujali mapenzi ya Mungu kabisa. Kwa nini ninaandika somo hili? Kwa sababu inanihuzunisha sana kwamba vijana wengi wanadanganywa na ‘motivational speakers’ wa namna hiyo. Wanasukumwa kutengneza malengo (goli) yao wenyewe na wahubiri hao, lakini kwa wengi malengo yao hayatatekelezwa kwa sababu mafundisho ya namna hiyo hayatokani na Biblia; wengine watawaambia wasikate tamaa lakini mwishoni watakata tamaa kwa sababu haya yote ni mambo matupu, ni upuuzi. Inawezekana wengine wataacha kumfuata Bwana. Na wahubiri hao wanachukua wajibu kwa ajili ya hiyo. (Kati maelfu mengi inawezekana wengine watafaulu, lakini watafaulu kwa sababu maisha ni maisha, siyo kwa sababu mafundisho hayo yanatokana na Mungu – ni jambo la kawaida tu kwamba kwa juhudi na uwezo wetu tunawezekana kufaulu.)
Yesu alifanya muujiza. Aliwalisha waume elfu tano kutokana na mikate mitano na samaki wawili. Ndipo tunasoma, “Kisha Yesu, hali akitambua ya kuwa walitaka kuja kumshika ILI WAMFANYE MFALME, akajitenga, akaenda tena mlimani yeye peke yake.” (Yoh.6:15). Kwa nini Bwana Yesu alijitenga? Inaonekana kuwa nafasi ya ajabu awe mfalme juu ya watu! Hapana! Watu wale walitaka kumfanya Yesu mfalme KWA AJILI YA FAIDA YAO TU ili wapate baraka za kimwili au za nje tu! KWA SABABU YA HIYO, waumini wengi wa siku hizi wanapenda sana ‘motivational speakers’! Vivyo hivyo kama wayahudi walipenda kumfanya Yesu mfalme wao! Msingi ni kujipendeza na siyo kujikana! Labda walisema, “Kumbe! Anafanya muujiza! Hatutahitaji cho chote tena! Yeye atatubariki kupita kiasi na sisi tutafanikiwa tu! ATABADILISHA MAZINGIRA YETU! Ataondoa maadui zetu Warumi! Ataboresha maisha yetu! Biashara yetu itafanikiwa, na yote tulilolitaka, yametimizwa! Twende tumfanye mfalme!” Je, na wewe unataka mwokozi wa namna hiyo awe mfalme wako? Kama ni hivyo, huwezi kumfuata Mwokozi Yesu Kristo! Huwezi kuwa mwanafunzi Wake – humjui. Yesu alikataa kabisa kuwa mfalme juu ya msingi wa kujipendeza kwa watu! Alijitenga na akaenda mlimani peke Yake. Je, utamfuata pale, pale jangwani, mlimani, pale ambapo hakuna cho chote ila Yesu tu na msalaba wake? Je, Yesu Mwenyewe tu anatosha kwako? Tunaimba, “Wewe tu ndiwe utoshaye.” Je, ni kweli kwako kila siku? Unataka nini? Unatafuta nini?
Bwana Yesu, Yeye aliye na macho yake kama mwali wa moto, huangalia na kuchunguza makasudi (motives) yetu kweli kweli yaliyofichwa ndani sana ya mioyo yetu! Yesu siyo ‘motivational speaker’. Watu wanaweza kusema hivi na hivi, wanaweza kuwa na hamu kwa ajili hivi na hivi, hata kumfuata Yeye, lakini Yesu anachunguza makusudi kweli kweli ya mioyo yetu! Yesu alisema, “Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu.” (Yoh.6:53). Baada ya kusema haya, imeandikwa, “Kwa ajili ya hayo wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma.” (Yoh.6:66). Wanafunzi hawa walikwazwa na mafundisho ya Yesu; walisema, “Neno hili ni gumu, ni nani awezaye kulisikia?” (Yoh.6:60). Labda walifikiri kupitia mafundisho ya Yesu hawatafanikiwa kuwavuta watu! Labda waliondoka kumtafuta mhubiri mwingine atakayefundisha mambo yale ambayo watu wanapenda kusikia na awezaye kufanikiwa kujenga ‘mega-church’! Je, Bwana Yesu alijaribu kuwashawishi warudi? Hapana. Yesu hakupaza sauti kuwatia moyo kwa kusema, ‘Rudini kwangu tu! Nitayaeleza yote! Hata nitawajulisha siri ya mafanikio!’ Badala yake, Bwana Yesu aliwauliza mitume waliobaki, “Je! Ninyi nanyi mwataka kuondoka?” Unaona? Maneno ya Yesu yanaingia mioyo yetu moja kwa moja kuuliza, “Unataka nini?” Yesu hatafuti kuwakusanya watu kujenga ‘umaarufu’ wake! Kwa maneno yake na kazi yake katika maisha yetu, Yesu Kristo anachunguza chunguza mioyo yetu mpaka makasudi yetu ya kiini kabisa yamefunuliwa. Wale watu ambao wanatengeneza ‘goli’ lao la binafsi kutokana na mafundisho ya ‘motivational speakers’ wanatayarisha njia ambayo inaweza kuwakwaza, na mwishoni, kuwasabibisha warudi nyuma!
Kwa nini wasemaji/wahubiri hao hawawalishi waumini kwa neno la Mungu? Imeandikwa, “Njia zote za mwanadamu huonekana sawa kwake, bali BWANA huupima moyo.” Na tena, “Njia zote za mtu huonekana safi machoni pake mwenyewe, BALI MAKUSUDI HUPIMWA NA BWANA.” (Mithali 21:2; 16:2). Hili ni kosa kubwa la wahubiri hao, yaani, wanawachochea waumini kutengeneza njia zao ambazo huonekana sawa machoni pao mwenyewe! Na wanaendelea kukosa zaidi kwa kudai ‘mbinu’ hiyo inaitwa ‘imani’ au ‘maono’! Lakini siyo imani, siyo ‘maono’, siyo mbinu– ni mchezo wa mawazo tu, ni mchezo wa saikolojia. Wahubiri hao wanawasukuma watu kucheza na mawazo yao tu. Kama wakitaka kuongelea maisha yetu ya baadaye, kwa nini hawatumii neno la Mungu,
“MTUMAINI BWANA kwa moyo wako wote wala USIZITEGEMEE AKILI ZAKO MWENYEWE; katika njia zako zote MKIRI YEYE, naye ATAYANYOOSHA  MAPITO YAKO. Usiwe mwenye hekima machoni pako mwenyewe, mche BWANA ukajiepushe na uovu.” (Mithali 3:5-7).
Unaona? Neno la Mungu linakuongoza kumtegemea Mungu kabisa, siyo mitazamo yako, au hata ‘maono’ yako ya binafsi kwa maisha yako ya baadaye! Huhitaji ‘kukiri maono’ yako kila wiki, au kila mwezi, au kila mwaka ili yatimizwe! Huhitaji kutoa jasho kwa sababu unajaribu jaribu kuamini Mungu atatekeleza maono yako au malengo yako! Neno la Mungu linaondoa mzigo huo huo, yaani, “Nitatengenza goli langu…nitaamini, sitakata tamaa…nitakiri goli yangu, sitashindwa…nitashika maono yangu mpaka yatimizwe, sitakata tamaa, sitakata tamaa, sitakata tama…” Lakini mwishoni wengi wanakata tamaa! Kinyume chake Mungu anakuongoza uingie katika raha Yake na pumziko Lake! Bwana asifiwe! Ni Habari Njema – siyo jasho la akili zetu! Ujumbe wa kutia moyo ni huo – Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote; mkiri Yeye katika njia zako zote! Hiyo ni njia ya imani. Hiyo ni njia rahisi mno! Hiyo ni njia ya baraka bila shaka! Tukijitoa Kwake na kuwa sikilivu, Yeye ni mwaminifu na ataipima mioyo yetu na makusudi yetu, na Yeye Mwenyewe atayanyoosha mapito yetu! Lakini hiyo haimaanishi njia Yake kwa ajili ya maisha yako ni sawa na ile uliyoitaka wewe! Kama Bwana Yesu alimwambia Petro, “Wakati ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga mwenyewe na kwenda utakako; lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka.” Lakini kama tukimpenda Mungu kuliko malengo yetu, kama tukiyatafuta mapenzi Yake na siyo ya kwetu, haitakuwa ngumu – itakuwa baraka kubwa tu! Kama Bwana wetu alisema, “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami NITAWAPUMZISHA.Jitieni nira yangu, MJIFUNZE KWANGU; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi MTAPATA RAHA nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:28-30).
Bwana Yesu hakuhubiri ‘injili ya baraka’, yaani, uje kwangu nami nitaboresha na kustarehesha maisha yako na utafanikiwa katika kila kitu! Yule mwanamke Msamaria alitaka Yesu amrahisishie na kustarehesha maisha yake akisema, “Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, WALA NISIJE HAPA KUTEKA.” Yule mwanamke hakuelewa maneno ya Yesu Kristo. Msamaria alifikiri juu ya mambo ya kimwili tu. Alitaka karama ya Mungu kwa ajili ya faida yake mwenyewe tu. Bwana Yesu hakufa msalabani kubadilisha au kuboresha mazingira yako, bali kukubadilisha wewe kwa ndani sana kabisa haijalishi mazingira ulipo! Kama vile Paulo alivyosema, “nimejifunza kuwa radhi na hali yo yote niliyo nayo.” Na wewe? Je, motivational speakers wanakufundisha uwe radhi na hali yo yote uliyo nayo? Au unaweza kuwa radhi tu kama malengo yako yakifanikiwa? Wewe unataka nini?
Bwana Yesu alipowajulisha mitume wake kwamba atakufa kwa udhaifu, Petro alimchukua Yesu na akamkemea! Kumbe! Jambo la ajabu! Mwanaadamu anamkemea Mungu! Petro hakuweza kuvumilia kamwe wazo la udhaifu, kutokufanikiwa – “Mwana wa Mungu atakufa msalabani! Haiwezekani!” Yesu akamwambia Petro, “Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana HUYAWAZI YALIYO YA MUNGU, BALI YA WANADAMU.” Maneno mazito sana! ‘Motivational speakers’ (wale wanaowasukuma wasikilaji wao kutengeneza malengo yao ya maisha ya baadaye) hufanya vivyo hivyo, yaani, kwa msingi hawayawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu – na wanajaribu ‘kumtumia’ Yesu kutimiza malengo yao wenyewe, vile vile Petro alivyotaka Yesu ajenge mfalme Wake duniani sawasawa na njia na malengo yake! Yesu aliendelea kuwaambia Petro na wanafunzi wake wote,
“Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate. Kwa kuwa mtu ATAKAYE KUIOKOA NAFSI YAKE, ATAIPOTEZA; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona. Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake?” (Math.16:23-26). Bwana Yesu alikufa msalabani kutusamehe dhambi zetu na kutuweka huru mbali na dhambi, kwa hiyo, “alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya NAFSI ZAO WENYEWE, bali KWA AJILI YAKE YEYE aliyekufa akafufuka kwa ajili yao.” (2 Wakor.5:15). Hilo ni kusudi la Mungu kwa ajili yako na yangu.
Na je. mtume Paulo alikuwa ‘motivational spealer’? Sidhani, hata kidogo. Nia ya Paulo na makasudi yake yalikuwa ya namna gani? Paulo alisema,
“Niliazimu nisijue neno lo lote kwenu ILA YESU KRISTO, NAYE AMESULIBIWA.”
Bwana asifiwe sana! Tunahitaji wahubiri wa namna hao siku hizi! Anaendelea,
“Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye KUSHAWISHI AKILI ZA WATU, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ILI IMANI YENU ISIWE KATIKA HEKIMA YA WANADAMU, bali katika nguvu za Mungu.” (1 Wakor.2:2-5).
Lazima ilimhuzunisha Paulo kuandika maneno hayo, “..sina mtu mwingine (kama Timotheo) mwenye NIA MOJA nami, atakayeiangalia hali yenu KWELI KWELI. Maana WOTE WANATAFUTA VYAO WENYEWE, sivyo vya Kristo Yesu.” (Wafilipi 2:20,21). Kama ilivyokuwa siku za Paulo, ni vivyo hivyo siku hizi – wahubiri wengi ‘wanatafuta vyao wenyewe, sivyo vya Kristo Yesu’. Kwa maisha yake ya kiroho Paulo anatangaza, “…NATENDA NENO MOJA TU; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, NIIFIKILIE MEDE YA THAWABU YA MWITO MKUU WA MUNGU KATIKA KRISTO YESU. Basi sisi tulio wakamilifu na TUWAZE HAYO.” (Wafilipi 3:13-15). Je, lengo lako na lengo langu, ni lile lile? Anasema, ‘tuwaze hayo.’ Jinsi ‘utakavyofanikiwa’ bila kuwa na nia ya Paulo, bila ‘kuwaza hayo’?
Hili ni neno la Mungu. SASA najisikia huru kukutia moyo, mpendwa msomaji, kufuata nia na makasudi ya Paulo. SASA unaweza kwa usalama kabisa kutengeneza lengo lako! Kwa Paulo, kumjua Yesu kulikuwa ya thamani na muhimu zaidi kuliko yote nyingine, “nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote NIKIYAHESABU KUWA KAMA MAVI ili nipate Kristo.” (Wafilipi 3:8). Je, tunaweza kusema yale yale, yaani, tunayahesabu yote kuwa kama mavi ili tupate Kristo? Je, hiyo ni nia yetu, mtazamo wetu, lengo letu? Hiyo haimaanishi mambo yote yenewe si kitu; inamaanisha mambo yote nyingine yanaonekana kama mavi kwangu KUYALINGANISHA NA KUMJUA YESU! Unaweza kusema hayo?
Tena Paulo anasema, “Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” Je, na sisi tunaweza mambo yote katika Yeye atutiaye nguvu? Au tunaweza kumsifu Mungu wakati malengo yetu ya binafsi yanapotimizwa tu au tunapofanikiwa tu?
Kama tunataka kutengenza mwelekeo wetu au nia yetu, tunalo neno jema kabisa,
Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu, ambaye …alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba.”
Kwa hiyo Paulo alisema, “Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida.” (Wafilipi 1:21).
Badala ya kuongea sana juu ya ‘lengo lako, kusudi lako duniani’, naamini ni muhimu zaidi sana kabisa kuliza, ‘Lengo la Mungu kwa ajili yangu ni nini?’ Lengo la uwepo wetu duniani ni nini? Jibu ni rahisi na wazi. Siyo siri. Toka mwanzo Mungu alitudhihirisha, “Mungu akasema, Na TUMFANYE MTU KWA MFANO WETU, KWA SURA YETU.” (Mwanzo 1:26). Na kupitia kifo na ufufuo wa Mwanwe, Mungu amelitekeleza LENGO LAKE, yaani, ili tuzaliwe toka juu, kuzaliwa na Mungu! Ili Yesu Kristo aishi ndani yetu, tuyadhihirishe maisha Yake duniani! (2 Wakor.2:15’ 4:10). “Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili WAFANANISHWE NA MFANO WA MWANA WAKE, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi.” (Warumi 8:29). Lengo la Mungu ni kuwa na watoto kwa mfano Wake, waliozaliwa na Roho Yake. Kwa nini ‘ametukirimia ahadi kubwa mno na za thamani’? Lengo la Mungu ni nini? Ni wazi – ‘ili kwamba kwa hizo TUPATE KUWA WASHIRIKA WA TABIA YA UUNGU.’ (2 Petro 1:4). Kwa ajili ya lengo lipi Mwana wa Mungu alikuja? Ni wazi, ‘Kwa KUSUDI HILI Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za Ibilisi’ ndani yako na ndani yangu! Mungu apewe sifa! Ujasiri wetu katika siku ya hukumu ni nini? Tumefanikiwa? Hapana. “Katika hili pendo limekamilishwa kwetu, ili tuwe na ujasiri katika siku ya hukumu; kwa kuwa, kama yeye alivyo, ndivyo tulivyo na sisi ulimwenguni humu.” (1 Yoh.4:17). Je, ulitaka kujua lengo lako hapo ulimwenguni?
Huo ni mwito mkuu. Hilo ni kusudi kuu la Mungu. Ndiyo, kuna elimu, na kazi, na biashara, na familia, na nyumba, na mwito, nkd, lakini mambo hayo yote yatapata nafasi yake kwa wakati wake kama tukijenga maisha yetu juu ya mwamba, Yesu Kristo.
Mungu ameshaitayarisha njia kwa ajili yako na mimi. ‘Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili tuenende nayo.’ (Waefeso 2:10). Jambo la ajabu! Paulo anatangaza, ‘Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa KWA KUSUDI LAKE.’ (Warumi 8:28). Je, ninajishughulisha na kulitimiza lengo langu? Paulo anasema, “UTIMIZENI WOKOVU wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.” Paulo anaendelea kutuambia kwa nini tunapaswa kufanya hivyo, “Kwa maana ndiye MUNGU ATENDAYE KAZI NDANI YENU, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa KULITIMIZA KUSUDI LAKE jema.” (Wafilipi 2:12,13). Unaona? Tayari Mungu anatenda kazi yake ndani yako kulitimiza kusudi LAKE! Ni afadhali kujishughulisha na kulijua kusudi lake kwa maisha yako kuliko kujaribu kutengeneza kusudi au lengo lako.
Kusudi la maisha ya milele ni nini? Ni wazi,
“Na uzima wa milele NDIO HUU, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yoh.17:3).
Kwa hiyo, “Bwana asema hivi, Mwenye hekima asijisifu kwa sababu ya hekima yake, wala mwenye nguvu asijisifu kwa sababu ya nguvu zake, wala tajiri asijisifu kwa sababu ya utajiri wake; bali ajisifuye na ajisifu kwa sababu hii, ya kwamba ANANIFAHAMU MIMI, NA KUNIJUA, ya kuwa mimi ni Bwana.” (Yeremia 9:23,24).

Post a Comment

0 Comments