VITA VYA KIROHO : ROHO ZITAWALAZO MAENEO



VITA VYA KIROHO : ROHO ZITAWALAZO MAENEO

Katika makala hii tutaangalia mafundisho yanayohusiana na kile wanachokiita “Roho za Kimaeneo”. Kulingana na mafundisho hayo, wanadai kuna roho chafu maalum ambazo zinatawala jamii, vijiji, miji, jiji au hata nchi nzima. Hiyo ina maana kwamba, roho hizo zinatawala katika eneo zima kulingana na jiografia ya eneo lenyewe; na hivyo huitwa “Roho za Maeneo”. Inaendelea kufundishwa zaidi kwamba eti hizi roho za maeneo zanao uwezo na mamlaka ya kuwabana watu katika giza, vifungo na dhambi kulingana na jiografia ya eneo lao. Kimsingi, zaidi ya hilo, hawa wanaohamasisha mafundisho hayo, wanatuambia kwamba hizi roho za maeneo zinao uwezo wa kushikilia jamii ndogo au miji kiasi kwamba Injili peke yake haiwezi kufaa, kupata kuingia wala kupendwa au kuenea katika eneo hilo hadi hapo hizi roho za kimaeneo zitakapotambulikana na kisha zikafungwa, zikazidiwa nguvu pamoja na kukemewa kwa njia ya maombi. Wanafundisha kwamba watu hawawezi kumjia Bwana, wakaokolewa na kukombolewa kutoka katika dhambi, giza, pamoja na vifungo mbalimbali, kwa idadi kubwa mpaka kwanza hapo tutakapotambua na kisha kuzifunga na kukemea nguvu za roho hizo za kimaeneo. Hivyo ndivyo wanavyosema na kuwafundisha watu.

Hiki ndicho kidokezo cha mafundisho yao kwa lugha rahisi kadiri iwezekanavyo, na nina hakika kwamba utakubali kuwa ikiwa mafundisho haya ni ya kweli, basi ni ya umuhimu mkubwa. Kuenea kwa Injili pamoja na kuokolewa kwa watu kunategemea ufahamu na matumizi ya mafundisho haya, ikiwa mafundisho hayo ni ya kweli! Jambo hili haliwezi kuwa swala la jinsi mtu aonavyo au tafsiri ya kibinafsi, kwa sababu litaathiri ufahamu wetu kuhusiana na jinsi Injili ilivyo, pamoja na lile alilolifanya Yesu pale Kalvari.

Kama ilivyo katika zile makala nyingine zilizopita, napenda kwanza niangalie yale ambayo Maandiko yanavyosema na kufundisha. Kwa hivyo, kwa muda huu, hatutaangalia Maandiko ambayo watu wanadhani wamepata kuyaona mambo hayo yakifundishwa. Jambo hili ni la msingi na lenye uzito mkubwa kiasi kwamba hatuwezi kuyaachia kwenye ubunifu au hisia za kibinadamu tu. Tunachotafuta ni maandiko ambayo mambo haya yanafundishwa dhahiri na kutajwa bayana.

Mambo haya yanafundishwa wapi ndani ya Agano Jipya?

Kwa jibu la urahisi na la ujumla kuhusiana na habari hiyo hapo juu ni – “Hakuna popote!” Hatuyapati mahala popote katika Agano jipya, mafundisho haya yahusuyo kutambua na kuzifunga roho za kieneo!
Yesu hakutumia au kufundisha mbinu hii.
Hakuna mahali popote tunaposoma kuwa Yesu aliibainisha roho iliyokuwa ikitawala eneo, kijiji au mji, na kisha akaifunga na kuikemea kabla hajaanza kuhubiri na kufanya miujiza mahali hapo.

Hakuna mahali popote ambapo Yesu aliwafundisha mitume wake au mtu mwingine yeyote kwamba Neno la Mungu linaweza kuwa na nguvu na mafanikio katika eneo fulani ikiwa kwanza utaibainisha roho ya lile eneo na kuifunga na kuzishinda nguvu zake kwa njia ya maombi. Kamwe hatusomi popote Yesu akiitumia au kuifundisha mbinu hii.

 Mitume hawakutumia au kufundisha mbinu hii.

Hakuna mahali popote pale katika Injili au kwenye Matendo ya Mitume ambapo tunasoma habari za mitume au mtu mwingine yoyote yule akitumia mbinu za jinsi hiyo katika kuineza Injili. Mtume Paulo alitembelea miji mingi sana ambamo kulikuwa na zinaa ya kutisha, mambo ya kimwili, uchawi pamoja na dhambi. Hakuna popote pale ambapo tunasoma juu yake akizitambua kwanza roho hizo katika miji hiyo ili aone ni aina gani ya roho za kimaeneo zinazotawala katika miji, wala hatusomi mahala popote pale na kuona akiomba juu ya roho za aina hiyo ili kwamba kazi ya Injili ipate kustawi.

Hakuna mahali popote pale ndani ya maandishi yao kwa makanisa au kwa watu binafsi, ambapo mitume hawa wamepata kutaja tu mbinu za jinsi hiyo, licha ya kuzifundisha. Yapo mahusia mbalimbali kwa ajili ya kuomba katika Agano Jipya. Lakini hakuna mahali popote pale ambapo mitume wanaelekeza kuwa roho za kimaeneo zina uwezo juu ya watu katika baadhi ya maeneo na kwamba watu hawana budi kuomba dhidi ya roho hizo na kuzivunja nguvu zake, ili kwamba Injili ipate kustawi na ili wanawake na wanaume wapate kuokolewa.
Hayapo mafundisho ya jinsi hiyo ndani ya Agano Jipya. Kwa msingi huu pekee, tunaweza, kwa usalama kabisa, kuyakataa mafundisho ya jinsi hii.

Lakini sasa, mtindo wa jinsi hii haufudishwi kwenye Agano la Kale wala hatuna hata mfano mmoja katika Agano la Kale, unaoelezea juu ya mtu yeyote anayezitambua roho za kimaeneo na kufunga nguvu zake kabla kazi ya Bwana haijakamilishwa ipasavyo. Kwa kweli, waandishi hao wa kisasa wanarejea katika maandishi fulani fulani ya Agano la Kale, na tutakwenda kuangalia maandishi hayo baadaye, lakini hata hivyo, hakuna hata andiko moja linalounga mkono mtindo huo na mbinu zao zinazoenezwa na waandishi hao.
Jukumu la Uongo

Wanawezaje walimu hawa wa siku hizi kusema, “Lazima uzitumie mbinu hizi ili kuhakikisha mafanikio ya uInjilisti katika ulimwengu”, wakati ambapo maandiko hayatushauri kufanya hivyo? Wanaweka jukumu juu ya watu we Mungu wakati ambapo maandiko hayaweki jukumu la jinsi hiyo. Kwa maneno mengine, wao huongezea maneno yao juu ya Neno la Mungu – na wakizitumia mamlaka zao juu ya watu wa Mungu, mamlaka ambazo hazitokani na Mungu. Hili ni jambo la hatari sana. Ni jambo moja kusema kuwa, kwa sababu maandiko hayawazuii kuzitumia mbinu hizo, kwa hivyo wao wanajisikia uhuru kuzitumia. (Hata hivyo, hoja hii si ya msingi, kwa sababu mafundisho yao yanagusa kweli za msingi za Injili na ufanisi katika kuenezwa kwake, hivyo wanapaswa kuonyesha kwa uhakika mambo hayo yanafundishwa wapi katika maandiko, kabla hawajafundisha na kuzitumia kanuni hizo). Lakini kwa kweli wanafundisha kanuni zao za lazima kwa ajili ya kueneza Injili. Huo ni udanganyifu na unaweza kuwapelekea watu wa Mungu, kutumbukia katika kuchanganyikiwa, vifungo pamoja na hatari iwapo watapokea na kuyafuata mafundisho ya jinsi hii.

Ikiwa mbinu hizi za kuzitambua na kuzifunga roho za kimaeneo ni za lazima kwa ajili ya kuleta mafanikio ya uenezaji wa Injili, kwa nini basi Yesu pamoja na mitume wake hawakufundisha wala kutufunulia mambo hayo? Tunaelezwa na hawa walimu wa kisasa kwamba maombezi dhidi ya mamlaka na uweza juu ya maeneo ya kijiografia, yanahitajika sana kabla Injili haijapenya katika maeneo hayo. Je, mitume walikuwa ni wajinga juu ya mbinu hizo? Au labda walishindwa kutufunulia kile kilicho cha lazima kwa ajili ya uenezi wa Injili, na kwa ajili ya wokovu wa nafsi za watu? Je kanisa litakuwa limeondolewa ukweli huu wa lazima kwa muda wa miaka 2000? Hapana! Kanisa halijanyimwa ukweli huu wa lazima, na bado Injili imeendelea kuenea muda wote huo kwa karne zote hizo, kama Yesu alivyosema Injili haina budi kuenea, hata bila kanisa kufundisha au kuzitumia mbinu hizo ambazo hawa walimu wa kisasa wamezibuni. Kutokea muda wa Matendo ya Mitume hadi kufikia siku hii ya leo, kumekuwepo na uamsho, maelfu ya watu wamerejea kwa Bwana kwa idadi kubwa, nao wameokolewa kutokana na dhambi, giza na vifungo vya shetani pasipo hata kujulikana kwa mbinu hizo, kufundishwa wala kuzitumia!

Kutamani “matokeo” kupita kiasi.
Lakini moja ya kusudio lao kuu hawa wahubiri na walimu wa kisasa ni kuona “matokeo”. Mmoja wa viongozi wa kanisa ambaye anaamini katika kutumia kanuni hizo amesikika akisema kuwa iwapo kanisa lake halitaongezeka kutoka washirika 1000 hadi kufikia washiriki 2000 ndani ya miaka miwili, basi hapo itakuwa ni kutokana na kushindwa kwao katika kujaribu kwa makini kufanya hivyo. Kwa maneno mengine, iwapo tutazitumia mbinu halisi basi tutegemee kanisani washirika kuongezeka mara mbili zaidi ndani ya miaka miwili! Watu hawa wanalifanya kanisa kuwa kana kwamba ni aina fulani ya biashara ambapo tunapaswa kuzitafuta kanuni bora zaidi ili kutoa matokeo na kufikia malengo. Hata makanisa mengi kwa sasa yameanza kutoa “maelezo ya umisheni” pamoja na malengo yao kwa ajili ya mafanikio yao. Mtindo wa aina hii kwa kazi ya Mungu, umeazimwa moja kwa moja kutoka kwa ulimwengu wa kibiashara. Hii yote inamdhalilisha Yesu Kristo ambaye ndiye kichwa cha kanisa lake ambaye ndiye aliyetuonyesha kwa neno lake jinsi itupasavyo kujishughulisha wenyewe. Mmoja wao amesema kwa uwazi kabisa kwamba wanavutiwa zaidi na yale “yanayofanya kazi” ( yaani, yanayoleta mafanikio au matokeo ) kuliko “yale yaliyo ya kweli”. Kwa hiyo basi, tayari wameanza kujenga msingi wa udanganyifu wao. Katika kujiondoa kwao kutoka katika miongozo iliyo sahihi ya Neno la Mungu, wao wamekuwa wakijiweka wazi kwa udanganyifu wa shetani; kadiri wanavyoendelea na kuzitumia mbinu na kanuni zinazoweza kuwaletea matokeo ya haraka na yenye kuvutia.

Yesu anaomba kwa Baba akisema “Neno lako ni kweli”, Yohana17:17. Sasa kama watu wa Mungu, sote tunatamani na kuomba kwamba Injili iweze kufikia na kuokoa nafsi za watu wengi watuzungukao na ulimwenguni kote. Lakini watu wa Mungu, maombi yetu, kazi zetu, pamoja na mafundisho yetu lazima yawe kulingana na neno la Mungu, ambako ndiyo kweli. Hamu yetu ya “kuona matokeo” isituongoze kuelekea kwenye kuikataa au kujitenga na Neno la Mungu kama lilivyofunuliwa katika maandiko; au kuanzisha mbinu zetu wenyewe au mtindo wa fikra kwa ajili tu ya kujipatia kile kinachoonekana kuwa ni “matokeo” ya haraka. Mengi ya mafundisho hayo ya kisasa yanasukumwa na mawazo ya “mafanikio” yakikusudia kutafuta kitu fulani “kinachofanya kazi” na hiyo ni “Mafanikio”. Hawa walimu wa kisasa wanaendelea kubuni mawazo mapya pamoja na mitindo ya kufundisha. Hakuna hata mmoja anayeweza kujihoji mwenyewe kuwa inakuwaje kila baada ya miaka michache kunahitajika “mitindo” mipya, katika mtazamo wa Kitheolojia – hii ni upepo mpya wa imani! Wala hakuna hata mmoja anayeweza kuuliza, kulitokea nini na ule upepo wa imani uliopita? Au kutambua kwamba kanisa halihitaji mtindo mpya katika mafundisho yake ya Imani isipokuwa ni marejeo kwa yale ambayo tayari yamefunuliwa vizuri katika maandiko. Ikiwa tutakuwa waaminifu, tutapaswa kuungama kwamba, mafundisho hayo mengi ambayo yanaendeshwa na wazo la mafanikio ni matokeo yanayotujia moja kwa moja kutoka kwenye mila za kibiashara za Marekani (U.S.A); mahala ambako kila kitu kinategemea malengo, matokeo pamoja na mafanikio. Na Wakristo zaidi sana huko Marekani wameazima akili hizo au wamechukua mtazamo na silka kutoka kwa ulimwengu na wameuingiza kanisani, umewapelekea kwenye ubunifu wa mafundisho na matendo ya kutatanisha.( Bila shaka, mimi sisemi kwamba, wazo la roho za kimaeneo linakuja kutoka kwenye desturi za kibiashara, lakini huu msukumo kwa ajili ya mafanikio – ambao umewapelekea Wakristo hawa kutumbukia katika ubunifu na udanganyifu).

Mwandishi na mwalimu ambaye ni mmoja wa waenezaji wakuu wa mafundisho haya anaelezea juu ya jambo ambalo nimeligusia hapo juu, kuhusiana na kukosekana kwa maandiko yanayounga mkono mafundisho haya. Katika utangulizi wa kitabu chake alichokiandika yeye mwenyewe kiitwacho “Territorial Spirits” (“Roho za Kimaeneo”; Sovereign World Ltd. Ó1991 C.P.Wagner), amesema kuwa, amewahi kutazama kwenye vitabu 100 huko kwenye seminari ya theolojia ambavyo vimezungumzia kuhusiana na somo la malaika na mapepo, ili aweze kugundua mafundisho yahusuyo roho za kimaeneo. Anaendelea kueleza kuwa, siku za leo ipo haja kubwa sana ya kufanya utafiti kwa ajili ya somo hilo. Lakini kwa nini tufanye utafiti? Je utafiti wa kwenye Biblia hautoshi? Je hatuna Biblia? Neno la Mungu halitoshi kutuelekeza kuhusiana na jambo kama hili la msingi? Kwa dhahiri kabisa sivyo hivyo, kwa kuwa yeye hawaaliki watu wafanye utafiti katika Biblia. Ijapokuwa kwa hakika anajaribu kutafuta ushahidi kwa ajili ya mafundisho hayo kwenye maandiko, kama tutakavyoweza kuona hapo baadaye, yeye anaenda sehemu nyingine ili kuona iwapo anaweza kupata uthibitisho kwa ajili ya ubunifu huu wa kigeni. Lakini anatuambia kwamba ni vitabu vitano tu kati ya 100 vilivyotaja kuhusiana na somo hilo la roho za kimaeneo, na kati ya hivyo vitabu vitano, ni vitatu tu ambavyo angalau vinasema chochote kinachoweza kusaidia. Lakini hakuna chochote kati ya vitabu hivyo ambacho kilistahili kujumuishwa katika kitabu chake. Hii haishangazi kwa vile mafundisho hayo hayamo pia katika Biblia – na mpaka sasa hakuna hata mmoja ambaye amebuni au kuyatumia kwa jinsi hiyo, kwa kadri nifahamuvyo. Kwa hiyo, katika kitabu chake hicho anajumuisha michango kutoka hasa kwa waandishi wa siku za leo ambao wanaoeneza mawazo ya jinsi hiyo. Wagner alikuwa anafanya utafiti juu ya kanuni za ukuaji wa kanisa na maombi, alipowafikia viongozi wa kanisa fulani ambao walikuwa wakifanya aina hii ya maombezi dhidi ya roho za kimaeneo. Hapo, ilimpelekea kuingia ndani zaidi ya mafunzo yake juu ya somo hili. Kama tulivyokwisha kuona katika makala nyingine iliyopita, watu hao wanapofanya utafiti wao hawaanzi kwa kusoma Biblia, isipokuwa wao huanza kwa kutegemea uzoefu wao wenyewe na “mafunuo ya kiroho” wanayoyapokea. Ndipo hutafuta maandiko ambayo huyalazimisha au kuyafanya yaunge mkono “mafunuo” waliyopokea. Nasi tutatazama maandiko hayo hapo baadaye. Lakini napaswa kusema kuwa, hata hao viongozi wa makanisa – ambao waliiamini imani hiyo ya kigeni, hawakubaliani wao kwa wao kuhusiana na mafundisho haya, na namna ambayo yanapaswa kutumiwa. Kwa vile hayaungwi mkono na maandiko ya Neno la Mungu, basi haishangazi kuona kwamba mmoja wa waenezaji wa mawazo haya ameamua kusema kwamba kwa kuwa Mungu ni mwenye enzi, basi anafunua mbinu mpya na bora kwa ajili ya uInjilisti wa ulimwengu mzima. Wanachomaanisha ni kwamba Mungu anaufunua kwao ufunuo huu usiopatikana katika Biblia, na hivyo wanajihesabia wenyewe mamlaka ya kitume! Yote hii inaonyesha jinsi wanavyoiacha imani, kwa vile wanayainua mafununuo yao na uzoefu wao juu ya neno la Mungu.
Hebu sasa tuyatazame kwa karibu yale yanayofundishwa na waandishi hawa wa kisasa kuhusu vita vya kiroho.

Post a Comment

0 Comments